MWENYEMACHO DOT COM

Yanapojiri Nilipo na Wewe Upo

Archive for July, 2007

BINTI WA KIMARI

Posted by Bob Sankofa on July 27, 2007

princess-wangui.jpgKuna wakati fulani Ndesanjo wa www.jikomboe.com aliwahi kuandika kuhusu kasichana kake ka kwanza kabisa, kaliitwa nani tena vile? Stela, bonyeza hapa usome zaidi.

Basi hata mimi pia nimewahi kuwa na “Stela” wangu pia, Wangui wa Kimari, mtoto toka Kenya huyu. Nilikutana naye wapi tena vile? Ahh, ni pale chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka ule wa 2004/2005. Wangui alikuwa akisoma Carlton University, Canada na alikuwa amekuja Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kitu kinaitwa Exchange Program (Kiswahili chake baadae).

Nakumbuka alinikaribisha chumbani kwake jioni moja, pale hall 3, kwa chai ya jioni. Nilikwenda, tulikuwa wawili tu chumbani lakini sikuweza kumwambia chochote. Akanitengenezeza kikombe cha chai, nikanywa.

Nakumbuka pia kuwa muda mwingi yeye ndiye alikuwa akiongea zaidi. Mimi nilikuwa nasikiliza zaidi. Aliniuliza napenda mziki wa aina gani, nikamwambia Afrika Magharibi, na muziki mwingine wowote wa kimapinduzi. Basi alikuwa na CD ya Michael Frant (Mcheki huyu jamaa kwenye Google, ni mtu matata sana), akaweka. Hii CD alikuja kunipa kama zawadi wakati alipokuwa akiondoka kurudi Canada.

Basi tukaendelea kunywa chai na kusikiliza ‘madongo’ ya Frant. Nilikuwa na nywele za msokoto (dredlocks) kipindi kile, akazishika na kuniambia kuwa alizipenda. Moyo ukanilipuka. Yeye pia alikuwa na nywele msokoto (Anazo hadi leo), nikamwambia nazipenda za kwake pia. Sikuweza kuendelea kuongea zaidi.

Kabla sijakaa sawasawa mwenzake ambaye walikuwa wakikaa chumba kimoja akarudi toka darasani, siku ile ikawa ndo imekufa tena. Shabaaaash, nilimlaani sana rafiki yule, kimoyomoyo lakini, kwani kaujasiri ka kusema jambo kalishaanza kuniingia. Read the rest of this entry »

Posted in Fotografia, Photography, Tanzania, Vijimambo | 16 Comments »

NYEPESI – 1

Posted by Bob Sankofa on July 21, 2007

10am311.jpgGarry Winogrand mpiga picha wa Kimarekani huyu, alifanya mtindo wa fotografia maarufu kama “Street Photogarphy”.Picha hii ni moja ya kazi zake katika mradi wa “Women are Beautiful”.

Kwa kiasi kikubwa kazi zake zilikuja kupata umaarufu zaidi baada ya kifo chake.

Inasemekana hadi siku anakufa, mwaka 1984, alikuwa na mikanda 2500 ya picha alizopiga ambayo ilikuwa bado haijasafishwa, alikuwa pia na filamu 6500 ambazo zilikuwa zimeshasafishwa lakini bado hazijahakikiwa, na pia alikuwa na picha 3000 ambazo zilikuwa tayari lakini hazikuwahi kuonyeshwa kwa watu wengi.

Kwa hesabu za haraka inasemekana Garry alikuwa akipiga picha 100 kila siku katika mitaa ya jiji la New York, hivyo kwa mwaka mzima aliweza kupiga picha 36,000, na kwa miaka 30 aliyoishi akifanya fotografia alipiga picha karibu milioni moja.

Wataalamu wa masuala ya fotografia wanasema iwapo unataka kuwa mwanafotografia wa mtindo wa “Street Photography” basi huna budi kujitoa kama ilivyokuwa kwa Garry. Tatizo ni kuwa ukijitoa namna hii unaweza ukawa mbali sana na jamii. Kwa mfano Garry hakuweza kuziokoa ndoa zake mbili zisivunjike. Alipenda fotografia kuliko wanawake. Upo?

Kwa undani zaidi tembelea http://www.photo.net/photo/winogrand

UHURU!

Posted in Fotografia, Vijimambo | 1 Comment »

TABIA 6 ZA WANAFOTOGRAFIA…

Posted by Bob Sankofa on July 21, 2007

his-name-is-innocent.jpgBaada ya kutumia kamera wanazoita “Point and Shoot” kwa muda mrefu hatimae nimefanikiwa kununua kamera yangu ya kwanza ya kitaalamu zaidi, wenyewe wanaiita DSLR, Canon 350D. Ile ya kwanza ilikuwa ni Sony DSC-P32. Na hii ni picha ya kwanza kabisa kupiga kwa kutumia kamera hii mpya.

Ningependa sana kuja kujitambulisha kwa watu kama mwanafotografia, sasa hivi bado sijafika huko. Nafanya kazi nyingi sana kwa wakati mmoja ili kuweka mkate mezani. Ukitembelea ukurasa wangu wa Mimi Ni Nani utaelewa nasema nini. Lakini nauona mwanga.

Huwa natembelea tovuti nyingi sana zinazohusiana na maswala ya fotografia. Sasa katika pitapita yangu nikakukutana na maandiko ya bwana mmoja anaitwa Richard Hann, jamaa ni mwanafotografia.

Richard ametoa kitu anachokiita “Tabia Sita za Wanafotografia Waliofanikiwa.” Anasema tabia hizi ni muhimu kupitiwa na kila mwanafotografia ambaye anahitaji kuendelea kukurutubisha kipaji chake.

Tabia zile sita ni hizi hapa:

      1. Siku Zote Wanakuwa na Mtazamo Chanya.

Richard anasema usijisumbue hata siku moja kumlaumu mtu mwingine au mazingira uliyomo kwa wewe kama mwanafotografia kushindwa kupata picha nzuri na zenye ubora. Kwa mfano usilalamike kwamba unashindwa kupata picha bora kwa sababu kamera yako ni ile ya bei rahisi. Ubora wa picha hauletwi na kamera bali jicho la mwanafotografia. Mwanafotografia ni msanii, beba kamera yako hata kama ni ya dola za kimarekani 20 na utengeneze sanaa. Read the rest of this entry »

Posted in Elimu, Fotografia, Photography, Tanzania | Leave a Comment »

TUMAINI!

Posted by Bob Sankofa on July 12, 2007

Mara Ngapi umesikia vilio toka Gaza?

Mara ngapi umesikia wazazi wa Kimarekani wanaolilia watoto wao waliopelekwa na Joji ‘Kichaka’ huko Iraq wakiwa hawana matumaini ya kurejea tena?

Mara ngapi umesikia kuhusu kilichotokea Rwanda, na sasa kinatokea tena Dafur na halafu wote tukajifanya kutokuwa na habari?

Mara ngapi umesikia kuhusu Robert Mugabe akiua watu wake kwa kisingizio cha kuwakomesha ‘mabwana’ wakubwa wa Magharibi?

Mara ngapi umesikia mwanasiasa wako akikupa ahadi za maisha matamu, kisha akajituniku mwenyewe?

Tazama,

Kungali na giza totoro sitakoma kuingoja nuru

Mjumbe atarejea tena.

Tumaini litarejea tena.

Posted in Fotografia, Siasa | 2 Comments »

SERIKALI YA BONGO NA BAJETI YA 2007/2008

Posted by Bob Sankofa on July 9, 2007

Wakati wa kampeni za urais wa Tanzania mwaka 2005, Rais wa sasa alikuwa na msemo wake maarufu wa “Maisha bora kwa kila Mtanzania”. Msemo ule niliufananisha na sahani hizi nzuri na mavijiko yake makubwa yanayoashiria kuwa mlo baada ya jamaa kuingia madarakani ungekuwa babkubwa.

Salaaalah, kumbe baba mwenye nyumba (Rais Kikwete) alikuwa akituahidi watoto wake (Watanzania) kwamba tutakula pilau na nyama ya kubanika (maisha bora) pasipo kuwasiliana na mpishi mkuu (Waziri wa Fedha, Mh. Zakhia Meghji) na kupata uhakika iwapo kiroba cha mchele, fungu la nyama, vitunguu na mafuta yapo.

Basi tumekabidhiwa sahani hizi na mavijiko haya (Ahadi hewa) tangu mwaka 2005 lakini chakula (maisha bora kwa kila mtanzania) bado havijaja na havitakuja karibuni. Sasa watoto (Watanzania) tumeanza kuvuta suruali ya baba (Rais Kikwete) kuuliza kulikoni, baba hana jibu anamuuliza mpishi mkuu (Mh. Meghji) kulikoni, mpishi mkuu anatukunjia ndita watoto (Watanzania na Vyombo vya habari vya ndani) eti tunamchonganisha na baba.

Mpishi mkuu anatoa jibu la haraka haraka, ili kulinda unga wake. Anasema, “Subirini dakika tano jamani (yani baada ya miaka mitano)”. Watoto tunakuja juu, kaka zetu (Vyombo vya habari) wanaenda mbele zaidi na kumvuta mpishi mkuu nywele. Mpishi mkuu anawauliza kina kaka “Uko wapi uvumilivu wenu (yani uko wapi uzalendo wenu), mbona ndugu zenu wa kambo (Vyombo vya habari vya nje) wanaweza kuvumilia, nyie mna njaa ya kiasi gani?”

Ukweli ni kuwa bajeti ya Bongo mwaka huu ni ya kufunga mikanda japo Mh. Meghji anakana hilo. Je Tuanze kulia kama wana wa Israel walipomlilia Musa wakidai kurudi utumwani Misri wakaendelee kula nyama wangali wakichapwa mijeledi mgongoni?

Picha hii nimeipiga kwenye kongamano fulani kule Msasani juma lililopita.

Posted in Fotografia, Siasa | Leave a Comment »

MWENYE MACHO AUZA PICHA YA KWANZA

Posted by Bob Sankofa on July 3, 2007

Hatimaye Mwenye Macho ameuza picha yake ya kwanza katika maisha yake ya upigaji picha kwenye jarida moja huko Ufaransa kupitia wakala wa picha aitwaye Cedric Galbe. Cedric Galbe ni mpiga picha wa Kifaransa ambaye ameanzisha tovuti iitwayo www.Galbe.com. Tovuti hii ni wakala wa wapiga picha toka Africa, Scandinavia, Mashariki ya Kati, na Marekani ya Kusini.

Picha aliyouza ni hiyo hapo juu ya mtaalamu wa hesabu aitwaye Ron. Ron alitoa mada kwenye mkutano wa TED uliofanyika Arusha mwezi uliopita. Mada yake ilikuwa inaonyesha ni kwa jinsi gani hesabu zinavyothibitisha kuwa maisha yalianzia Afrika. Kwa habari zake zaidi tembelea www.jikomboe.com, Ndesanjo alimwandika vizuri zaidi. Mimi sikumwelewa sawasawa kwani mimi na hesabu hatukuwahi kuwa marafiki hata kidogo.

Mpaka wakati mwingine, naelekea benki mara moja kuona kama dola zangu zimeingia.

Posted in Fotografia | 8 Comments »

KUNA UTAMADUNI MPYA NYUMBANI

Posted by Bob Sankofa on July 1, 2007

Unamkumbuka Rhymson, mmoja wa waasisi wa Hip Hop hapa Tanzania? Alikuwa na kundi la mwanzo kabisa la mtindo huo wa muziki, likiitwa KWANZA UNITY. Siku hizi Rhymson ni mwafrika aliyezaliwa upya na anaitwa Zavara.Zavara alikuwa ughaibuni kwa takribani miaka isiyopungua kumi, huko Kanada na Marikani. Huko alikuwa akifanya shughuli za mziki pamoja na filamu. Sasa baada ya kipindi chote hicho amerejea hapa nyumbani na kuungana na “Waafrika” wa hapa ili kuweza kupeleka jahazi la mziki wa Hip Hop mbele, katika mstari ulionyooka.

Zavara pamoja na “Waafrika” kadhaa wa hapa akiwemo msanii na mwanaharakti aitwaye Mejah wameungana na kuanzisha mradi uitwao “Uma Project”. Huu ni mradi wenye lengo la kukusanya vijana wa “Kiafrika” wenye ndoto ya kufanikiwa katika sanaa bila kuisahau asili yao. Vijana hawa wengi wao ni wale wasio na uwezo wa kifedha kuweza kufanikisha ndoto zao.

Uma Project huandaa tamasha kila jumamosi ya mwisho wa mwezi na kuwakutanisha vijana pale British Council, Dar es Salaam. Sasa jana lilikuwa ni tamasha la tatu na lilipewa jina la “WEWE NI NANI?”. Jina hili lina dhumuni la kumfanya kila binadamu kujiuliza kuhusu uwepo wake kabla hujafanya jambo na kuhakikisha iwapo unajitambua. Tamasha la mwezi uliopita liliitwa “USWAZI WAPI?”.

Katika tamasha la jana kulikuwa kuna wachoraji, wanamuziki, wapiga picha mgando na za video, watu wa masuala ya mitindo ya mavazi (Wakiongozwa na Merinyo wa Afrika sana), na wengine wengi.

Kila kitu kilikuwa poa sana ila nilivutiwa sana na sanaa ya kuchora grafiti ukutani. Sanaa hii inasimamiwa na kuongozwa na Mejah, yeye ni mtaalamu wa sanaa hii, aliisomea kule New York, Marikani. British Council wamejitolea ukuta ambao vijana wa kitanzania wanapatiwa fursa ya kuandika grafiti kuelezea hisia na mawazo yao. Picha hizi za grafiti hudumu kwa muda wa mwezi mmoja halafu hufutwa na kuta kupakwa rangi nyeupe tayari kwa watu kuchora tena katika tamasha linalofuata.

Elimu ya Grafiti hutolewa bure pale, rangi pia hutolewa bure na jamaa wa British Council. Kwa kweli huu ni utamaduni mpya hapa nyumbani, na ni kitu poa sana kwani unawafanya vijana wa kiafrika kujitambua katika kila wanachijatahidi kufanya.

Posted in Sanaa | 3 Comments »